Nigeria: Wanawake 42 watekwa nyara na wanamgambo wa Kiislamu

Aliyekuwa kiongozi wa Boko Haram.

Wanawake wasiopungua  42 wametekwa nyara na wanamgambo wa Kiislamu wenye itikadi kali wakati wa shambulio katika jimbo la Borno kaskazini mashariki mwa Nigeria, wenyeji waliliambia shirika la habari la Associated Press Jumatano.

Waasi waliwashambulia watu hao walipokuwa wakikusanya kuni katika wilaya ya Jere, jimbo la Borno, ambalo ni kitovu cha uasi, uliodumu kwa muda wa miaka 14, na ulioanzishwa na kundi la itikadi kali linalojulikana kama Boko Haram, kwa mujibu wa mjumbe wa Kikosi Maalum cha Usalama cha eneo hilo aliyejitambulisha kwa jina la Abba.

Wenyeji pia walisema waathiriwa hao walikuwa wanatoka katika kambi ya wakimbizi wa ndani katika wilaya jirani ya Mafa na wamekuwa wakiuza kuni ili kujikimu kimaoisha, huku hali ngumu ya kiuchumi nchini Nigeria chini ya rais mpya ikizidi kuongezeka.

Waliozungumza na shirika la habari la Associated Press walisema waasi wamedai fidia ya naira 50,000 ( swa na dola 55 za Marekani), kwa kila mwanamke, ingawa wenyeji walikuwa wakijadiliana, wakitaka kulipa kiasi kidogo cha fedha, ili wanawake hao waachiliew huru.

Utekaji nyara huo wa hivi punde zaidi ulitokea saa chache baada ya wanamgambo kuvizia vikosi vya usalama vinavyolinda wakulima katika eneo hilo, kulingana na Abba na kundi moja la usalama la eneo hilo.

Boko Haram, wanamgambo waliokulia nchini Nigeria, walianzisha uasi mwaka 2009 ili kupigana dhidi ya elimu ya nchi za Magharibi na kuanzisha sheria ya Kiislamu ya Shariah nchini humo.

Takriban watu 35,000 wameuawa na watu milioni 2.1 wamekimbia makazi yao kutokana na ghasia hizo za itikadi kali, kulingana na takwimu kutoka kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini Nigeria.