Mwanahabari mwanamke raia wa Ukraine afariki akiwa gerezani nchini Russia

  • VOA News

Wanachama wa chama cha waandishi wa habari wa Ukraine wakishikilia picha za waandishi wa habari watatu wanaofungwa na Russia, moja ya picha hizo ni ya Victoria Roshchyna, Oktoba 17.2023. Picha ya AP

Mwandishi wa habari mwanamke aliyekamatwa na Russia alipokuwa akiripoti mashariki mwa Ukraine amefariki akiwa chini ya ulinzi, maafisa wa Ukraine walitangaza Alhamisi.

Viktoria Roshchyna mwenye umri wa miaka 28, alikuwa ameshikiliwa kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Kifo chake katika gereza la Russia kilitangazwa na msemaji wa kitengo cha wafungwa wa vita wa Ukraine.

Msemaji huyo, Petro Yatsenko, alisema ni “mapema sana kuzungumzia mazingira ya kifo chake.”

Lakini chombo cha habari cha Russia, Mediazona kimeripoti kwamba mwanahabari huyo alifariki alipokuwa akihamishiwa Moscow kutoka gerezani huko Taganrog, karibu na mpaka wa Ukraine.

Afisa wa idara ya ujasusi ya kijeshi ya Ukraine alisema Roshchyna alitarajiwa kuachiliwa katika mpango wa kubadilishana wafungwa, na inaaminika alikuwa amehamishiwa Moscow kwa lengo hilo alipofariki.