Msumbiji yaomboleza kifo cha kiongozi wa upinzani Dhlakama

Marehemu Afonso Dhlakama

Rais wa Msumbiji Filipe Nyusi anasema taifa limekumbwa na msiba mkubwa kutokana na kifo cha kiongozi wa Afonso Dhlakama aliyefariki Alhamisi akiwa na umri wa miaka 65 katika mji wa Gorongosa kutokana na ugonjwa wa kisukari.

Kiongozi huyo wa kundi la zamani la waasi la Renamo aliongoza vita vya msituni tangu Msumbiji ilipojinyakulia uhuru mwaka 1975 hadi makubaliano ya Amani yalipofikiwa mwaka 1992.

Katika taarifa iliyotolewa na ikulu ya Msumbiji Ijumaa imeeleza kuwa Rais Nyusi amesema ni pigo kubwa kwake kwani walikuwa wamefikia makubaliano ya hivi karibuni ya kutanzua matatizo ya nchi, kuleta mabadiliko ya katiba na kumaliza uhasama wa miaka mingi kati ya chama tawala cha Frelimo na Renasmo.

Dhlakama alishindwa katika kila uchaguzi wa urais alioshiriki tangu mwaka 1992, na alikuwa anajitayarisha kugombania kiti cha urais kwa mara nyingine 2019 dhidi ya Rais Nyusi.

Alichukuwa uamuzi huo baada yakufikia makubaliano mapya ya kusitisha mapigano mwaka 2016 na kukubali kurudi katika jukwa la kisiasa. Mashirika ya kutetea haki za binadamu wanamlaumu kwa kusababisha mauaji na ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu katika ngome yake kati kati ya Msumbiji.