Mkutano wa NATO kuanza mjini Washington Jumanne

  • VOA News

Nembo ya NATO nje ya ukumbi wa mkutano mjini Washington DC.

Mataifa wanachama wa NATO Jumanne wanaanza mkutano wao mjini Washington DC, ajenda kuu ikiwa ni uvamizi wa Russia dhidi ya Ukraine.

Viongozi wa NATO wanatarajiwa kukamilisha mpango wa juhudi za kila taifa kuisaidia Ukraine kwa msaada wa kijeshi, katika kuratibu mpango wa upelekaji vifaa kwa jeshi la Ukraine. Msaada huo unatarajiwa kuongezeka kutokana na ahadi mpya za silaha, ulinzi wa anga na misaada mingine, ili kukidhi maombi ya viongozi wa Ukraine ambao wanasema wanahitaji misaada zaidi ili kulinda anga yao dhidi ya mashambulizi ya Russia, pamoja na kuwasukuma nyuma wanajeshi wa Russia kutoka mstari wa mbele.

Mkutano huo pia utazungumzia hatua ya Ukraine kuelekea kwenye uanachama wa NATO. Ajenda nyingine kwenye kikao hicho kinachoongozwa na waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken ni kuhusu wanawake, amani na usalama. Katibu mkuu wa NATO Jens Stoltenberg atahutubia kikao na viongozi wa ulinzi pamoja na maafisa kutoka mataifa wanachama wa NATO, kujadili namna ya kuboresha utengenezaji silaha, wakati vita vya Ukraine vikiendelea. Rais wa Marekani Joe Biden pia anatarajiwa kutoa hotuba yake baadaye, kwenye kongamano hilo la 75 tangu kuanzishwa kwa NATO.