Mfalme Charles agunduliwa kuwa na saratani

  • VOA News

Mfalme Charles wa Uingereza na mkewe Malkia Camilla baada ya kutoka hospitali

Mfalme wa Uingereza, Charles III, amegunduliwa kuwa na saratani na ameanza matibabu, Kasri ya Burkingham ilisema Jumatatu, bila kutoa maelezo zaidi kuhusu aina ya saratani aliyo nayo.

Baada ya chini ya miezi 18 ya utawala wake, Mfalme Charles mwenye umri wa miaka 75 atasitisha majukumu yake ya umma, lakini ataendelea na shughuli za serikali, na hatakabidhi majukumu yake ya kikatiba kama mkuu wa taifa kwa yeyote, taarifa ya Kasri ya Buckingham ilisema.

Mfalme Charles alipimwa na kupatikana na ugonjwa huo wakati alipolazwa hospitali kwa siku tatu mwezi uliyopita kwa matibabu ya tezi dume.

Taarifa inasema vipimo aliyofanyiwa Mfalme akiwa hospitali kutibiwa tezi dume, ndio vilibaini ugonjwa huo lakini haikutoa maelezo yoyote kuhusu "aina ya saratani iliyogunduliwa."

Muda mfupi baada ya kugunduliwa na ugonjwa huo, Mfalme Charles alianza kupata matibabu akiwa nyumbani.

Kasri iliongeza kuwa mfalme "amechagua kuweka wazi hali yake ya afya ili kuepusha uvumi na kwa matumaini kwamba, kufanya hivyo kutasaidia umma kuelewa zaidi ugonjwa huo na wale wote duniani ambao wameathiriwa na saratani."

Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak alimtakia Mfalme Charles afueni kamili na ya haraka.

"Sina shaka kuwa atarejelea afya kamili baada ya muda mfupi, na najua nchi nzima itakuwa ikimtakia heri," alisema.