Mazungumzo ya sitisho la mapigano ya Gaza yaanza upya mjini Cairo, Misri

  • VOA News

Rais wa Misri Abdel Fattah al-Sisi akiwa na kiongozi wa Qatar Emir Sheikh Tamim bin Hamad al-Thani na katibu mkuu wa Ligi ya mataifa ya kiarabu ,Ahmed Aboul Gheit .Picha ya maktaba

Ripoti zinasema kuwa mazungumzo kuhusu sitisho la mapigano huko Gaza yanaanza tena Jumapili mjini Cairo, Misri, yakileta pamoja wapatanishi wa Misri na Qatar, wakitarajia kupata majibu kutoka kwa Hamas kuhusu mkakati wao wa karibuni zaidi kuelekea lengo hilo.

Afisa wa ngazi ya juu kwenye utawala wa Biden amesema Jumamosi kwamba Israel tayari imekubali pendekezo lililotolewa. “Kwa sasa maamuzi yapo mikononi mwa Hamas, wakati tukiendelea kuzingatia hilo iwezekanavyo, “amesema afisa huyo, aliyezungumza na wanahabari bila kutaka kutambulishwa, kwa kuwa hajarahusiwa kutoa taarifa hizo kwa umma.

Iwapo makubaliano yatafikiwa, basi kutakuwa na sitisho la mapigano la wiki 6, pamoja na kuachiliwa kwa mateka wanaoshikiliwa na Hamas, waliopo hatarini, wakati misaada zaidi ya kibinadamu ikiruhusiwa kuingia Gaza. Hamas wameendelea kushikilia msimamo wao kwamba sitisho la muda la mapigano ndio mwanzo wa kumaliza mapigano kabisa, kulingana na vyanzo vya Misri, na afisa mmoja wa Hamas.

Shirika la habari la AFP limeripoti Jumapili kwamba afisa wa ngazi ya juu wa Hamas amesema kwamba kuna uwezekano wa sitisho la mapigano ndani ya saa 24 hadi 48 zijazo, iwapo Israel itakubali masharti ya Hamas.