Mashirika ya Umoja wa Mataifa yaonya wakimbizi walioambukizwa Mpox nchini DRC wako katika hatari ya kifo

  • VOA News

Wagonjwa wakimsikiliza daktari nje ya kituo kinachotoa matibabu ya Mpox huko Goma Kaskazini, DRC Agosti 17, 2024. Picha na AFP

Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanaonya kwamba wakimbizi na jamii zilizohamishwa kutoka kwa makazi yao nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na nchi nyingine za Afrika walioambukizwa mpox wako katika hatari kubwa ya ugonjwa na kifo, kwa sababu ya mazingira ambayo wanalazimika kuishi.

Shirika la afya duniani (WHO) linasema visa 42 vinavyoshukiwa kuwa vya ugonjwa wa mpox vilibainishwa miongoni mwa wakimbizi katika jimbo la Kivu Kusini, moja ya majimbo yaliyoathiriwa zaidi na ugonjwa huo.

Visa vilivyothibitishwa na vinavyoshukiwa vya aina mpya ya Clade 1B pia vimerikodiwa miongoni mwa wakimbizi katika Jamhuri ya Congo na nchini Rwanda.

“Visa vinavyoshukiwa vimeripotiwa katika majimbo yanayoathiriwa na mzozo ambayo yanahifadhi wengi kati ya wakimbizi wa ndani milioni 7.3, ” Dr Allen Maina, mkuu wa afya ya umma kwenye shirika la UNHCR, alisema Jumanne.

Wiki mbili zilizopita, WHO ilitangaza mpox kuwa dharura ya afya ya umma duniani kufuatia kuongezeka kwa ugonjwa huo mbaya nchini DRC na katika nchi nyingine 11 za Afrika.