Mashirika ya kiraia Tunisia yataka wagombea waliokataliwa waruhusiwe kuwania uchaguzi wa urais

Rais wa Tunisia Kais Saied akitoa hotuba katika hafla ya kuapishwa kwa serikali mpya katika Ikulu ya Carthage nje ya mji mkuu wa Tunis, Februari 27, 2020.

Ombi lililotiwa saini na watu mashuhuri wa Tunisia na mashirika ya kiraia lilichapishwa Jumamosi wakitaka wagombea waliokataliwa waruhusiwe kugombea katika uchaguzi wa urais wa Oktoba 6

Likiwa limetiwa saini na makundi 26 ikiwa ni pamoja na Wanasheria Wasio na Mipaka na taasisi ya Tunisian Human Rights League, lilikaribisha uamuzi wa mahakama ya kiutawala wiki hii wa kuwarejesha kwenye nafasi wagombea watatu ambao walikuwa wameenguliwa.

Wagombea hao ni Imed Daimi, ambaye alikuwa mshauri wa rais wa zamani Moncef Marzouki, waziri wa zamani Mondher Zenaidi na kiongozi wa chama cha upinzani Abdellatif Mekki.

Watatu hao walikuwa miongoni mwa wagombea 14 waliozuiliwa na halmashauri ya kusimamia uchaguzi ya Tunisia, ISIE kugombea katika uchaguzi huo.