Mashambulizi ya Lebanon yalikuwa pigo kubwa- asema kiongozi wa Hezbollah

  • VOA News

Kiongozi wa Hezbollah, Hassan Nasrallah akihutubia taifa kutoka mahala pasipojulikana. Sept. 19, 2024.

Kiongozi wa Hezbollah, Hassan Nasrallah, Alhamisi amekiri kwamba shambulizi la wiki hii ndani ya Lebanon kupitia vifaa vya mawasiliano vya kundi hilo, lilikuwa pigo kubwa, huku akisema kuwa Israel ilivuka mipaka hatari kwa kutekeleza operesheni hiyo.

Takriban watu 32 walikufa, na wengine 3,000 kujeruhiwa, pale wapiganaji wa Hezbollah wasiokuwa na habari, pamoja na watu wengine walipokuwa wakijaribu kuwasiliana kupitia vifaa maarufu kama pager, lakini badala yake vikalipuka vikiwa mikononi mwao.

Mashambulizi hayo ya Jumanne na Jumatano yanaaminika kutekelezwa na Mossad, ambalo ni shirika la kijasusi la Israel, ingawa Israel haijakiri wala kukanusha madai hayo. Kufuatia tukio hilo, Lebanon imepiga marufuku ubebaji wa vifaa vya mawasiliano vya pager na walkie talkie, kwa watu wanaotumia uwanja wa kimataifa wa Beirut, wakati wakiwa kwenye ndege.

Ni marufuku pia kubeba vifaa hivyo kwenye mikoba ya abiria na mizigo mingine ya ndege. Wakati akiwa mjini Paris, waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken alisema kuwa Marekani haingependa kuona ongezeko la mizozo ndani ya Labanon, kwa kuwa huenda ikahujumu juhudi za kufikia sitisho la mapigano kati ya Israel na Hamas kwenye Ukanda wa Gaza.

Baadhi ya wataalam wa usalama kutoka Mashariki ya Kati na Marekani wameambia vyombo vya habari vya Marekani wiki hii kwamba wanaamini kwamba mawakala wa Israel walinasa kasha la vifa vya pager vilivyokuwa vikipelekwa Lebanon, kutoka kampuni moja ya Budapest, mji mkuu wa Hungary, na kisha wakaviweka vilipuzi kabla ya kuwasilishwa kwa kundi la Hezbollah.