Marufuku iliyowekewa radio moja ya Burkina Faso yaondolewa na serikali

Picha ya Kapteni Ibrahim Traore anayeongoza utawala wa kijeshi wa Burkina Faso

Uongozi wa kijeshi wa Burkina Faso umesema Jumatatu  kwamba kituo kimoja cha redio kilichokuwa kimepigwa marufuku kutokana na kufanya mahojiano yaliyokuwa na matusi kwa viongozi wapya wa kijeshi wa Niger kinaweza kurejea kwenye shughuli zake.

Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, kituo cha Radio Omega kilipigwa marufuku Agosti 10, lakini waziri wa mawasiliano Rimtalba Jean Emmanuel Ouedraogo, ametangaza kuondolewa wa marufuku hiyo hapo Jumapili. Ameongeza kusema kwamba serikali ilitathmini kwa kina ombi lililotolewa na kituo kinachofuatilia vyombo vya habari vya Burkina Faso.

Kituo hicho awali kilifanya mahojiano na Ousmane Abdoul Moumouni ambaye ni msemaji wa kundi jipya la Niger linalofanya kampeni ya kumrejesha madarakani rais aliyechaguliwa kidemokrasia Mohamed Bazoum, na aliyeondolewa na walinzi wake wa kijeshi madarakani.

Radio Omega ni sehemu ya kampuni ya utangazaji ya Omega inayomilikiwa na mwanahabri ambaye pia aliwahi kuwa waziri wa mambo ya kigeni wa Burkina Faso Alpha Barry.