Marekani na Uingereza zashambulia ngome kadhaa za Wahouthis nchini Yemen

Picha hii iliyochapishwa na kamandi ya Jeshi la Marekani Januari 22, 2024, inayoonyesha uharibifu uliosababishwa na mashambulizi ya Marekani na Uingereza dhidi ya ngome za Wahouthis Yemen

Marekani na Uingereza zilishambulia ngome 36 za waasi wa Kihouthi nchini Yemen, katika siku ya pili ya mashambulizi makali dhidi ya makundi yanayoungwa mkono na Iran kufuatia shambulio dhidi ya wanajeshi wa Marekani wiki moja iliyopita.

Mashambulizi hayo ya Jumamosi yalilenga ghala za kuhifadhi silaha zilizofichwa, mifumo ya makombora na zana nyingine zilizotumiwa na Wahouthis kushambulia meli katika Bahari ya Sham, wizara ya ulinzi ya Marekani imesema, ikiongeza kuwa ililenga maeneo 13 kote nchini Yemen.

Ni mashambulizi ya hivi karibuni katika mzozo unaozidi kupamba moto Mashariki ya Kati tangu shambulio la Oktoba 7, wakati kundi la wanamgambo wa Palestina la Hamas lililipoishambulia Israel kutoka Ukanda wa Gaza, na kuchochea vita ambavyo vimepelekea makundi yanayoungwa mkono na Iran kufanya mashambulizi dhidi ya ngome za Marekani na Israel.

Msemaji wa jeshi la Wahouthis Yahya Sarea ameapa kwamba watalipiza kisasi dhidi ya mashambulizi hayo ya Marekani na Uingereza.