Marekani inafanya operesheni kuwaondoa wafanyakazi wake ubalozi wa Haiti

Haiti inaendelea kuwepo katika hali ya dharura huku Marekani ikiondoa wafanyakazi wasio muhimu katika ubalozi wa Marekani huko Haiti

Operesheni hiyo ilikuwa ishara ya karibuni ya matatizo wakati ghasia za magenge zikitishia kuiangusha serikali ya Haiti

Jeshi la Marekani limesema leo Jumapili kuwa limefanya operesheni nchini Haiti kuwasafirisha wafanyakazi wasio muhimu wa ubalozi kutoka nchini humo na kuongeza wanajeshi wa Marekani kuimarisha usalama wa ubalozi, wakati taifa hilo la Caribbean likikabiliwa na hali ya hatari.

Operesheni hiyo ilikuwa ishara ya hivi karibuni ya matatizo ya Haiti wakati ghasia za magenge zikitishia kuiangusha serikali na kusababisha maelfu kukimbia makazi yao. Usafiri huu wa ndege wa wafanyakazi ndani na nje ya ubalozi ni utaratibu wetu wa kawaida wa kuimarisha usalama kwa ofisi za ubalozi duniani kote, na hakuna raia wa Haiti aliyekuwemo ndani ya ndege ya jeshi, ilisema taarifa ya kamandi ya kusini ya jeshi la Marekani.

Haiti iliingia katika hali ya dharura Jumapili iliyopita baada ya mapigano kuongezeka huku Waziri Mkuu Ariel Henry akiwa Nairobi akifuatilia makubaliano ya kwa uchelewesho wa muda mrefu wa ujumbe ambao unaungwa mkono na Umoja wa Mataifa.

Kenya ilitangaza mwaka jana kuwa itaongoza kikosi cha polisi lakini miezi kadhaa ya mivutano ya kisheria katika taifa hilo la Afrika Mashariki imekwamisha ujumbe huo kusonga mbele.