Mahakama ya Kenya yabatilisha amri ya ukataji miti iliyotolewa na Rais

Picha ya maktaba ya msitu unaochomeka. British Columbia Julai 24, 2023.

Mahakama moja mjini Nairobi imekatiza furaha ya wafanyabiashara wa mbao baada ya kubatilisha amri ya rais William Ruto  ya kuwaruhusu kuanza tena ukataji miti kwenye misitu.

Julai 2 mwaka huu wakati akizungumza kwenye mji wa Molo katika Kaunti ya Nakuru, Ruto alitoa amri ya kubatilisha sheria iliyozuia ukataji miti, wakati ikikosolewa vikali kwa kuweka maslahi ya kibiashara mbele ya utunzaji wa mazingira.

Kwa mujibu wa gazeti la The Standard, Jaji wa mahakama ya Mazingira na Ardhi Oscar Angote ameirejesha sheria inayozuia ukataji miti, kufuatia kesi iliyowasilishwa na shirika la mawakili nchini Kenya, LSK, ya kupinga amri ya Ruto.

Awali Ruto alieleza nia yake ya kuongeza viwango vya misitu hadi asilimia 28 kutoka asimia 8.8 iliyopo sasa, kama hatua ya kulinda Kenya dhidi ya athari za mabadiliko ya hali ya hewa.