Israel yaishambulia Lebanon kwa siku ya pili, huku idadi ya vifo ikivuka 560

  • VOA News

Wakazi wakikagua eneo lililoshambuliwa na Israel katika vitongoji vya kusini mwa Beirut, Septemba 24, 2024. Picha ya AP

Israel Jumanne ilishambulia tena ngome za kundi la wanamgambo la Hezbollah nchini Lebanon, huku idadi ya vifo kutokana na mashambulizi ya anga tangu Jumatatu ikiongezeka hadi 564, pamoja na watu 1,835 waliojeruhiwa.

Kwa ujumla, Israel imesema ilishambulia ngome 1,600, huku maafisa wa afya wa Lebanon wakisema watoto 50 waliuawa katika mashambulizi hayo, pamoja na wanawake 94.

Jeshi la Israel limesema mashambulizi yake ya Jumanne katika vitongoji vya kusini mwa Beirut yalimuua Ibrahim Muhammad Kobeisi, aliyetambulishwa na Israel kama kamanda mkuu wa Hezbollah ambaye alikuwa anasimamia mifumo ya makombora ya Hezbollah.

Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi limesema “limekasirishwa na kuuzunishwa” na mashambulizi ya Israel ambayo yaliua wafanyakazi wake wawili.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres aliuambia mkutano wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa wakati wa ufunguzi, “Sote tunapaswa kushtushwa na kuongezeka huku kwa mapigano. Lebanon ipo katika hatari. Wananchi wa Lebanon, wananchi wa Israel na wananchi wa dunia hawawezi kustahamili Lebanon kuwa Gaza nyingine,” ambapo Israel na wanamgambo wa Hamas wamekuwa wakipigana kwa takriban mwaka mmoja.