Israel imetangaza upanuzi wa vita vyake dhidi ya Hamas

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu

Ofisi ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu imesema baraza la mawaziri la usalama limeidhinisha hatua hiyo Jumatatu.

Israel imetangaza Jumanne upanuzi wa vita vyake dhidi ya Hamas ili kujumuisha lengo la kuwawezesha wakaazi wa kaskazini mwa Israel kurejea katika majumbani walikohamishwa kutokana na mapigano kati ya wanajeshi wa Israel na wanamgambo wa Hezbollah katika mpaka wa Israel na Lebanon.

Ofisi ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu imesema baraza la mawaziri la usalama limeidhinisha hatua hiyo Jumatatu jioni. Hezbollah, mshirika wa Hamas, ilianza mashambulizi yake ya karibu kila siku muda mfupi baada ya vita vya Gaza kuanza, na kuwalazimisha maelfu ya watu kuyakimbia makazi yao.

Hezbollah, ambayo kama Hamas inaungwa mkono na Iran, imesema itasitisha mashambulizi hayo kama kutakuwa na makubaliano ya kusitisha mapigano kwa Gaza. Juhudi za kufanikisha sitisho la mapigano zimeendelea kwa miezi kadhaa, huku maafisa wa Marekani, Misri na Qatar wakijaribu kutafuta misingi itakayokubaliwa na wote, Israel na Hamas.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken anasafiri kwenda Misri leo Jumanne huku juhusi zikiendelea kuwashirikisha washirika muhimu wa kikanda katika Mashariki ya Kati, kutathmini pendekezo la kusitisha mapigano.