Hezbollah wanatafuta mwili wa kamanda wao, kiongozi wa Hamas ameuawa akiwa Iran

Kiongozi wa juu zaidi wa Iran Ayatollah Ali Khamenei (kulia) akizungumza na kiongozi wa wanamgambo wa Hamas Ismail Haniyeh (katikati) katika mkutano mjini Tehran July 30 2021

Wanamgambo wa Hezbollah wenye makao yao nchini Lebanon, wamesema kwamba wanautafuta mwili wa kamanda wao wa ngazi ya juu baada ya Israel kusema kwamba aliuawa katika shambulizi la anga mjini Beirut.

Katika taarifa, kundi la Hezbollah limesema kwamba Fouad Shukur alikuwa katika jengo lililopigwa na kombora la Israel siku ya Jumanne.

Israel imesema kwamba Shukur alipanga shambulizi la anga la Jumamosi, lililoua watoto 12 kwenye uwanja wa mpira katika sehemu inayokaliwa na Israel, ya Milima ya Golan.

Shukur anaaminika kuwa mshauri wa kijeshi wa kiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah, na amekuwa kiungo muhimu sana katika kundi la Hezbollah ambalo limeorodeshwa na Marekani kuwa kundi la kigaidi.

Marekani ilimuwekea vikwazo mwaka 2015 na amekuwa akitafutwa na Marekani kwa kuhusika na shambulizi la kambi ya jeshi la Marekani mjini Beirut mwaka 1983.

Kiongozi wa Hamas ameuawa akiwa Tehran

Kwingineko kundi la wanamgambo wa Hamas limesema leo Jumatano kwamba shambulizi la Israel limemuua kiongozi wake Ismail Haniyeh, akiwa mjini Tehran, alipokuwa amekwenda kuhudhuria sherehe ya kuapishwa kwa rais mpya wa Iran.

Taarifa ya Hamas iliyochapishwa kwenye mtandao wa Telegram imesema kwamba Haniyeh aliuawa katika nyumba mjini Tehran.

Kikosi cha Ulinzi wa Mapinduzi cha Iran kimesema kwamba mmoja wa walinzi wa Haniyeh pi aameuwawa katika shambulizi hilo la mapema asubuhi, na kwamba uchunguzi unafanyika.

Israel haijasema lolote kuhusu tukio hilo.

Kifo cha Haniyeh kimejiri karibu miezi 10 baada ya kundi la Hamas, linaloungwa mkono na Iran, kushambulia kusini mwa Israel na kuua watu 1,200 na kuwateka nyara 250.

Israel ilijibu shambulizi hilo kwa kuanzisha operesheni ya kijeshi huko Gaza ambapo kulingana na wizara ya afya ya Gaza, zaidi ya wapalestina 39,400 wamefariki. Idadi hiyo haitofautishi wapiganaji na raia.