Hatima ya Rigathi Gachagua wa Kenya inatarajiwa kuidhinishwa na wabunge

Naibu Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua.

Hatua hiyo inafuatia kura ya kihistoria wiki iliyopita katika baraza kuu la bunge la taifa kumng'oa madarakani Rigathi Gachagua

Baraza la Seneti la bunge la Kenya linatarajiwa kupiga kura leo Alhamisi kuamua iwapo linamuondoa Naibu Rais Rigathi Gachagua kutoka madarakani katika sakata la kisiasa ambalo halijawahi kutokea nchini humo.

Baraza la Seneti litarajiwa kuchukua uamuzi wake katika siku ya pili ya kesi ya kumng'oa mamlakani naibu wa Rais William Ruto. Hatua hiyo inafuatia kura ya kihistoria wiki iliyopita katika baraza kuu la bunge la taifa, kumng'oa madarakani Gachagua kwa mashtaka 11 yakiwemo ufisadi, kutumia vibaya mamlaka yake na kufanya siasa za kikabila.

Kesi katika seneti ilianza Jumatano baada ya kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 59, ambaye pia anajulikana kama “Riggy G”, kushindwa katika kesi kadhaa za mahakama kusitisha utaratibu huo. Mwanasiasa huyo aliwasili bungeni leo Alhamisi, muda mfupi kabla ya kikao kufunguliwa na anatarajiwa kutoa ushahidi katika utetezi wake baadaye.

Gachagua anakanusha mashtaka yote, na hakuna kesi ya jinai iliyofunguliwa dhidi yake, lakini ataondolewa madarakani kulingana na sheria, kama Seneti inaidhinisha mashtaka yake.