Biden apongeza ushirikano mpya wa usalama na ulinzi kati ya Marekani na Vietnam

  • Abdushakur Aboud

Rais Joe Biden wa Marekani akaribishwa na Waziri Mkuu wa Vitenam Nguyen Phu Trong, mjini Hanoi kwa kukagua Gwaride la Heshima.

Rais Biden alizungumzia mkutano huo alipokuwa mjini Hanoi, ambako alikutana na wajumbe wa serikali mapema Jumapili na kukubaliana kuimarisha ushirikiano wa usalama na ulinzi na Vitenam, pale Washington inapojaribu kuimarisha na kupanua mtandao wake wa washirika katika kanda ya Asia na Pasifik kutokana na kuongezeka kwa ushawishi wa Bejing katika kanda hiyo.

"Tulizungumza juu ya utulivu. Tulizungumza kuhusu namna ya kuhakikisha nchi za ulimwengu wa tatu, samahani, kanda ya kusini mwa dunia inaweza kupata mabadiliko. Nchi zinaweza kupata maendeleo na wala si mfarakano hata kidogo," amesema Rais Biden.

Rais Joe Biden akihudhuria mkutano na waziri mkuu wa Vitenam Nguyen Phu Trong mjini Hanoi

Washington na Bejing zinavutana kuhusiana na masuala kadhaa ya kimataifa, na Biden anaituhumu China kwa kujaribu kugeuza muelekeo wa kimataifa kwa maslahi yake binafsi.

"Jambo moja linalofanyika hivi sasa ni China imeanza kubadili baadhi ya kanuni za mchezo, kwa upande wa masuala ya biashara na mambo mengine. Na jambo ninalotaka kufanya siyo kuitenga China. Bali ni kuhakikisha kanuni hazibadilishwi katikati ya njia, ikiwa ni katika usafiri wa anga au usafiri wa baharini, inahusiana na kuheshimu kanuni za kimataifa," amesema Rais Biden

Washington imewekeza kwa nguvu katika kuimarisha ushirikiano na washirika kama sehemu ya mkakati wake wa usalama na ulinzi katika kanda ya Bahari ya Hindi na Pasifik – Indo-Pacific- ikiwa ni pamoja na majadiliano ya usalama kati ya mataifa manne yanayohusisha India Australia na Japan. Na mkataba wa ulinzi wa AUKUS, kati ya Uingereza na Australia.

Rais Joe Biden wa Marekani akizungumza na waandishi habari mjini Hanoi, Vietnam.

Kwa upande wa Vitenam Biden amesifu ushirikiano wa karibu na Vitenam wakati mataifa haya mawili yamefikia makubaliano ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa ulinzi kutokana na ushindani mkubwa kutoka China.

Kwenye mkutano wake na waziri mkuu Nguyen Phu Trong, viongozi hao walishuhudia kutiwa saini mkataba mpya wa ushirikiano wa ulinzi, ikiwa ni ushirikiano wa juu wa kidiplomasia kati ya Hanoi na Washington.

Waziri Mkuu Trong, amemshukuru Biden kwa mchango wake wa kuimarisha uhusiano kati ya Marekani na Vietnam.

"Muktadha wa ushirikiano mpya uko chini ya misingi ya ushirikiano iliyokuwepo kati ya nchi zetu mbili na sasa tunaimarisha kufikia kiwango kipya cha kuongeza ushirikiano katika nyanja za uchumi, biashara na uwekezaji katika mwelekeo wa ubunifu na kukarabati mambo kwa misingi ya uhusiano wetu wa pamoja," amesema waziri mkuu Trong.

Mkutano kati ya ujumbe wa Marekani na Vietnam kati ya Rais Joe Biden na Waziri Mkuu Nguyen Phu Trong mjini Hanoi.

Biden alielekea Hanoi moja kwa moja kutoka mkutano wa G20 ambao haukuweza kukubaliana juu ya mpango wa kumaliza utumiaji wa mafuta ghafi na uliogubikwa na mgawanyiko mkubwa kuhusu uvamizi wa Russia nchini Ukraine, ingawa walikubaliana juu ya taarifa ya mwisho ambayo lugha ilipunguzwa ukali.