Balozi Ali Karume apokonywa uanachama wa CCM

Ali Karume, aliyekuwa mmoja wa viongozi wakuu wa CCM Zanzibar.

Chama tawala cha CCM  Zanzibar kimemfuta uanachama kada wake, Balozi Ali Karume na kumtaka arejeshe kadi ya chama hicho.

Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi la Tanzania, hatua hiyo imefikiwa zikiwa zimepita siku 23 tu tangu Balozi Karume alipopewa barua ya onyo Juni 15, kabla ya juzi kuibuka tena akisisitiza kauli zake kwamba hakuna demokrasia ndani ya CCM.

Kabla ya hatua hiyo, Karume alihojiwa na kamati ya maadili ya CCM tawi la Mwera, akahojiwa na kamati ya maadili ya CCM Jimbo la Tunguu na alihojiwa na kamati ya maadili ya CCM Wilaya ya Kati na kupewa barua ya onyo akiwekwa chini ya uangalizi wa miezi mitatu.

Akitangaza uamuzi wa kikao hicho Katibu Mwenezi wa CCM mkoa Kusini Unguja, Ali Timamu Haji amesema umefikiwa baada ya kumjadili na kupokea mapendekezo kutoka vikao vya chini kuhusu mwenendo na tabia ya mwanachama huyo.

"Tumepokea mapendekezo kutoka vikao mbalimbali vya chini na tumevipitia na sisi kama chama Mkoa kwa mujibu wa katiba ya CCM ya mwaka 1977 toleo la mwaka 2022 ibara ya 89 (4) Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa inatupa nguvu hiyo,” amesema.

Amesema ibara ndogo ya 14 (14) inaelekeza kuwa kumuachisha au kumfukuza uanachama mwanachama yoyote endapo itathibitika kuwa endapo tabia na mwenendo wake vinamuondolea sifa za uanachama na mwanachama anayefukuzwa anaweza kukata rufaa kwa kamati kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa.