Chepngetich avunja rikodi ya dunia ya marathon wanawake

  • VOA Swahili

Ruth Chepngetich akimaliza wa kwanza kwenye mbio za Chicago. Jumapili Oktoba 13, 2024,

Ruth Chepngetich mwanariadha wa Kenya amevunja rikodi ya mbio za marathon wanawake kwa karibu dakika mbili, aliposhinda mbio za marathon za Chigago Jumapili akitumia muda wa saa 2 dakika 9 sekunde 56.

Chepngetch mwenye umri wa miaka 30 anakua mwanamke wa kwanza kushinda mara tatu mbio za Chicago akivunja pia rikodi ya dunia ya 2:11:53 iliyowekwa na Muethiopia Tigst Assefa mwaka 2023 mjini Berlin.

“Nina furaha sana, Ninajivunia, kwani hii ilikua ndoto yangu ambayo iliyofanikiwa,” amesema Chepngetich bingwa wa dunia wa marathon mwaka 2019.

“Nimepigania sana kuvunja rikodi ya dunai na nimefanikiwa.”

Chepngetich aliyeshinda pia mbio za Chicago 2021 na 2022 alimtunza ushindi huo Kelvin Kiptum, aliyeweka rikodi ya dunia upande wa wanaume mwaka 2023, miezi kadhaa kabla ya kifo chake katika ajali ya gari akiwa na umri wa maika 24.

Muethiopia Sutume Kebede aliyekua akifanya mazowezi na Kiptum alichukua nafasi ya pili katika mashindano ya Jumapili akitumia saa 2 dakika 17 sekunde 32 akifuatwa na Irine Cheptai wa Kenya kwa nafasi ya tatu.