Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatano, Septemba 18, 2024 Local time: 01:44

Umoja wa Mataifa waweka vikwazo vya silaha kwa mwaka mwingine kwa pande hasimu za Sudan


Mkuu wa jeshi la Sudan Jenerali Abdel Fattah al-Burhan na kamanda wa RSF Mohamed Hamdan Dagalo
Mkuu wa jeshi la Sudan Jenerali Abdel Fattah al-Burhan na kamanda wa RSF Mohamed Hamdan Dagalo

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa kauli moja limeongeza kwa mwaka mwingine vikwazo vya silaha kwa pande zinazopigana katika jimbo la Darfur nchini Sudan, ambako vita kati ya majenerali hasimu vimepamba moto katika miezi ya hivi karibuni.

Mjumbe wa Sudan amepongeza hatua hiyo lakini amelitaka baraza hilo kuchukua hatua zaidi na kulichukulia vikwazo kundi la wanamgambo la Rapid Support Forces (RSF), kundi hasimu la jeshi la serikali ya Sudan.

“Kundi la wanamgambo kwa ujumla wake, hakika lazima liorodheshwe, sababu limekidhi masharti yote,” Balozi Al-Harith Idriss al Harith Mohamed alisema.

RSF imeteka eneo kubwa la Darfur, na vita vimekuwa vikiendelea tangu mwezi Mei katika mji mkuu wa Darfur Kaskazini, El Fasher, mji pekee wa jimbo la Darfur uliotekwa na RSF.

Jeshi la Sudan limeshtumu mara kadhaa Umoja wa Falme za Kiarabu kwa kutoa silaha na zana nyingine kwa RSF kupitia nchi jirani ya Chad. Umoja wa Falme za Kiarabu umekanusha vikali tuhuma hizo.

Forum

XS
SM
MD
LG