Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Septemba 19, 2024 Local time: 19:15

Tanzania: Kesi ya kikatiba ya kupinga kusainiwa mkataba wa bandari kuanza kusikilizwa Julai 2023


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (Courtesy Photo Michuzi Blog)
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (Courtesy Photo Michuzi Blog)

Mahakama Kuu nchini Tanzania kanda ya Mbeya Julai 20 mwaka huu inatarajiwa kuanza rasmi kusikiliza  kesi ya kikatiba ya kupinga kusainiwa kwa mkataba wa bandari, iliyofunguliwa na baadhi ya wananchi mkoani Mbeya.

Wananchi hao wanadai wana wawakilisha wenzao wanaopinga baadhi ya vipengele vya mkataba wa uwekezaji katika bandari ya Dar es salaam, nchini Tanzania, kati ya serikali na kampuni ya uwekezaji kutoka Dubai ya DP World.

Baadhi ya wanasheria wanao wawakilisha wananchi katika kesi hiyo ni pamoja na Boniface Mwabukusi, Livino Ngalimitumba, na Philip Mwakilima ambao wanadai kwamba mkataba huo hauna maslahi mapana kwa taifa isipokuwa kugawa rasilimali za nchi kwa wawekezaji.

Wakili Boniface Mwabukusi amedai kwamba shauri hilo limefunguliwa kwa hati ya dharura hivyo kuiomba mahakama kutoa tafsiri halisi ya maombi yao na kuweka zuio la kuanza utekelezaji wa mkataba huo.

Wakili Mwabukusi anasema: “Wao wanawadanganya wananchi kwamba eti siyo mkataba ni makubaliano.....”

Wananchi ambao ndio walalamikaji katika kesi hiyo ni pamoja na wakili Emannuel Chengula, Alphonce Lusako, Raphael Ngonde na Frank Nyalusi.

Lusako ambaye ni mlalamikaji anasema: “Sisi kama wananchi raia wa kawaida kabisa kwenye nchi yetu…”

Jaji Dastan Ndunguru anayesikiliza kesi hiyo ameiahirisha hadi Julai 14 mwaka 2023, kwa ajili ya Jamhuri kutoa majibu na baadaye waleta maombi kujibu ikiwa watakuwa na hoja na ndipo itakapoanza kusikilizwa Julai 20 mwaka huu.

Hilo limejiri baada ya mwendesha mashtaka mkuu wa serikali Hangi Chang'a na mwenzake Ayubu Sanga kuiomba mahakama kupanga tarehe nyingine kuwasilisha majibu ya serikali.

Baadhi ya wanaharakati walikuwepo mahakamani hapo mkoani Mbeya wakati wa kufunguliwa kwa kesi hiyo.

Bob Chacha Wangwe ambaye ni mwanaharakati alisema: “…Sisi tumesafiri kutoka sehemu mbalimbali kuja kuungana na kina Alhonce...”

Sakata linalohusisha uwekezaji katika bandari ya Dar es salaam lilianza kushika kasi hivi karibuni baada ya kutangazwa mwekezaji huyo mpya, kampuni ya DP World kutoka Dubai huku wengi wanaopinga wakidai kwamba hawapingi mkataba bali baadhi ya vipengele vilivyomo ndani ya mkataba huo.

Wakati huo huo serikali kupitia viongozi mbalimbali akiwemo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wamekuwa wakitolea ufafanuzi juu ya uwekezaji katika bandari ya Dar es Salaam na kuondoa dhana kwamba upo kwa ajili ya kuuza raslimali za nchi.

Forum

XS
SM
MD
LG