Zelenskyy asema Ukraine ipo tayari kutengeneza silaha zaidi mwaka 2024 kwa ajili ya vita vya Russia

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy.

Tukitazama mbele kwa mwaka 2024, rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy katika  hotuba yake ya kila siku kwa taifa Jumamosi amesema kwamba Ukraine “inajiandaa kutengeneza silaha zaidi mwaka ujao.”

“Tunashirikiana na washirika wetu katika kutafuta masuluhisho yanayohitajika kwa kila mwanajeshi wa Ukraine, pamoja na taifa letu kwa ujumla,” amesema kiongozi huyo. Katika siku ya mwisho ya mwaka huu Jumapili, jeshi la anga la Ukraine limesema kwamba limeangusha droni 21 miongoni mwa jumla ya 49 zilizorushwa na Russia.

Taarifa zimeongeza kusema kwamba Ukraine Jumamosi ilikuwa ikikabiliana na mashambulizi ya droni kutoka Russia kwenye mji mkuu wa Kyiv. Makombora mawili ya Russia yanaripotiwa kupiga kati kati mwa mji wa Kharkiv Jumamosi na kujeruhi takriban watu 21, kulingana na maafisa wa Ukraine.

Mashambulizi ya Russia huko Kharkiv yamefuatia yale ya anga ya Ukraine mapema Jumamosi kwenye mji wa Russia wa Belgorod, karibu na mpaka wa mataifa hayo mawili. Wizara ya Ulinzi ya Russia imesema kwamba takriban watu 21, wakiwemo watoto 3 waliuwawa huku wengine 110 walijeruhiwa kwenye shambulizi hilo la Ukraine la Belgorod.