Uingereza yadai jeshi la Russia linaendelea kujiimarisha kwa ajili ya vita vya Ukraine

Picha ya mamluki ya kundi la Wagner ambao baadhi wanasemekana kujiunga na jeshi la Russia.

Wizara ya Ulinzi ya Uingereza imesema Jumapili kwamba Rosgvardia, ambalo ni jeshi la Russia, linalenga kuimarisha rasilimali zake pamoja na vikosi, kutokana na migogoro ya ndani nchini Russia, iliyosababishwa na vita vya Ukraine.

Ripoti ya kila siku kutoka wizara hiyo imeongeza kusema kwamba sehemu moja ya kundi la mamluki la Wagner, ilijiunga na jeshi hapo Oktoba, ikifuatiwa mwezi huu na kundi la uasi la Donetsk People’s Republic, au Vostok.

Moscow imekuwa ikifanya juhudi za kuvunja kundi la eneo lililojitenga la Kaskad ambalo hujihusisha na operesheni za droni, wakati ikijitahidi kuweka sehemu ya kundi hilo chini ya jeshi la kitaifa la Rosgvardia, ripoti zimeongeza.

Hatua hizo pamoja na amri ya Russia kwa jeshi lake wakati wa msimu wa joto ya kutumia silaha nzito, huenda zikasababisha ongezeko la mashambulizi ya Russia kwenye vita vya Ukraine, wizara hiyo imesema.

Wakati huo huo silaha ya maangamizi ya Russia imeripotiwa kugonga mji wa mashariki mwa Ukraine wa Pokrovsk Jumamosi, takriban kilomita 80 kaskazini magharibi mwa Donetsk, gavana wa eneo hilo ameripoti kupitia ukurasa wake wa Telegram.