Ramaphosa kuzuru Misri mwishoni mwa wiki kwa ajili ya mzozo kati ya Isreal na Gaza

Rais wa Africa Kusini Cyril Ramaphosa akiwa na Rais wa Marekani Joe Biden kwenye picha ya maktaba.

Rais wa Afrika kusini Cyril Ramaphosa anatarajiwa kuhudhuria Mkutano  wa Amani mjini Cairo Jumamosi, kujadili jinsi ya kumaliza mzozo wa Israel na Gaza.

Kiongozi huyo alialikwa na mwenzake wa Misri ili kushiriki kwenye mazungumzo hayo, ambayo yatajikita zaidi kwenye kuenea kwa mzozo kati ya Israel na ukanda wa Gaza. Ofisi ya Rais ya Afrika Kusini imesema kwamba mkutano huo ni kuhusu misaada ya kibinadamu pamoja na kutoa wito wa kuanza tena kwa mazungumzo ya amani.

Taarifa zimeongeza kuwa Ramaphosa alikuwa na wasiwasi mkubwa kuhusu mashambulizi dhidi ya raia, watu kukoseshwa makazi pamoja na mzozo wa kibinadamu huko ukanda wa Gaza.

Awali Ramaphosa alisema yupo tayari kuwa mpatanishi kwenye mzozo huo, akiongeza kuwa taifa lake linaweza kuwa mfano wa uzoefu wa utatuzi wa mizozo barani Afrika na kwingineko.