Rais wa Iran asifu mataifa ya Afrika wakati wa ziara ya waziri wa mambo ya kigeni wa Burkina Faso

Rais wa Iran Ibrahim Raisi akiwa kwenye gari lake, kwenye picha ya maktaba.

Rais wa Iran Ebrahim Raisi Jumatatu amezipongeza nchi za kiafrika kwa kupinga ukoloni , wakati wa ziara ya waziri wa mambo ya nje  wa Burkina Faso nchini humo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, Raisi aliyasema hayo wakati wa mkutano na waziri wa mambo ya nje wa Burkna Faso, Olivia Rouamba mjini Tehran, akiyasifu mataifa ya kiafrika kwa kupinga ukoloni ingawa hakuitaja Ufaransa moja kwa moja.

Burkina Faso na Mali ambazo zilikuwa koloni za Ufaransa zinaongozwa na makundi ya kijeshi ambayo yalivunja uhusiano wao na taifa hilo, na kisha kuimarisha uhusiano wao na Russia.

Nchini Niger ambako kundi la kijeshi lilifanya mapinduzi Julai imekuwa ikishuhudia maadamano ya kuvitaka vikosi vya Ufaransa nchini humo viondoke. Kupitia taarifa iliyondikwa kwenye tovuti rasmi ya rais wa Iran, Raisi alisifu kile alichokitaja kuwa mwamko mpya.

Wakati wa kikao na Rouamba, Raisi alielezea azma ya Iran kushirikiana na mataifa rafiki ya kiafrika. Rouamba kwa upende wake alisema kwamba Burkina Faso iko tayari kuimarisha ushirikiano wake na Iran.

Katika miaka ya karibuni, Iran imekuwa ikiimarisha uhusiano na bara la Afrika kama jihudi ya kupunguza kutengwa, pamoja na kupunguza makali ya vikwazo ilivyowekewa tangu 2018 baada ya Marekani kujiondoa kwenye mkataba wa nyuklia. Hapo Julai Raisi alizitembelea Kenya, Uganda na Zimbabwe.