Mtoto wa kiume wa Rais wa Somalia alaumiwa kusababisha ajali Uturuki

Rais wa Somali Hassan Sheikh Mohamud picha ya maktaba. Nov. 20, 2023.

Uturuki imeomba maelezo kutoka kwa Somalia baada ya mtoto wa kiume wa rais Hassan Sheikh Mahmoud kuondoka nchini humo kufuatia ajali mbaya ya barabarani, iliyohusisha gari lake la kidiplomasia, kulingana na afisa mmoja wa Uturuki.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, Mohamed Hassan Sheikh Mahmoud alikuwa akiendesha gari la ubalozi wa Somalia nchini Uturuki hapo Novemba 30, ambapo aligonga pikipiki katikati mwa mji mkuu wa Istanbul, na kumjeruhi vibaya dereva wa pikipiki hiyo, kulingana na vyombo vya habari vya Uturuki.

Afisa aliyetoa taarifa hizo amesema kuwa Hassan hakuwa na hadhi ya kidiplomasia na hivyo hakuwa na idhini ya kuendesha gari lenye nambari za kidiplomasia. Mtoto huyo wa Rais wa Somalia inasemekena aliondoka Uturuki Decemba 2 baada ya kuhojiwa na polisi, wakati mtu aliyegongwa kwa jina Yunus Emre Gocer mwenye umri wa miaka 38 alikuwa hospitali.

Hata hivyo aliaga dunia Decemba 6, na kupelekea kutolewa kwa hati ya kimataifa ya kukamatwa dhidi ya Hassan, kulingana na ofisi ya mwendesha mshtaka.