Mtandao wa kusafirisha watu kwa njia haramu kutoka Uzbekistan wagunduliwa na Marekani

Wahamiaji wakitembea karibu na uzio wa waya kwenye mpaka wa Marekani na Mexico wa Rio Grande .July 16, 2023.

Utawala wa Biden umesema Jumanne kwamba umegundua na kusitisha mtandao uliyokuwa unalenga kusafirisha watu kwa njia haramu kutoka Uzbekistan kuingia  Marekani, na kuongeza kwamba mtu mmoja kwenye mtandao huo anahusishwa na kundi la kigaidi la kigeni.

Taarifa kutoka kwa Baraza la Kitaifa la Usalama imesema kwamba maafisa wa Marekani hawaamini kwamba raia wa Uzbekistan waliotumia mtandao huo walikuwa na uhusiano na magaidi, na wala hawakuwa na mpango wa kufanya mashambulizi ya kigaidi. Taarifa hiyo hata hivyo haikutaja kundi la kigaidi linaloshukiwa, lakini afisa mmoja wa Marekani ambaye hakutaka kutambulishwa ameambia AP kuwa ni lile la Islamic State.

Marekani imeshirikiana na serikali za kigeni katika kukamata na kushikilia watu wanaohusika kwenye mtandao huo, akiwemo anayeshukiwa kujihusisha na kundi la kigaidi. Idara ya upelelezi ya FBI ambayo pia imekuwa ikichunguza kisa hicho imesema kwamba haijapata tishio lolote la kigaidi miongoni mwa wahamiaji waliokamatwa.