Japan na Ufilipino kubuni ushirikiano wa kijeshi ili kudhibiti ushawishi wa China

Boti ya walinzi wa bahari wa Ufilipino ikipita mbele ya meli ya walinzi wa Japan, kwenye maji ya bahari ya South China Sea.

Japan na Ufilipino wametangaza kuanza kwa mashauriano ya mkataba wa kijeshi utakaoruhusu vikosi vyao kutumwa kwenye maeneo ya kila mmoja ,hatua ambayo wachambuzi wanasema huenda imechochewa na mwenendo wa kichokozi wa China kwenye maji ya bahari yanayozozaniwa.

Waziri mkuu wa Japan Fumio Kishida amekutana na rais wa Ufilipino Ferdinand Marcos Jr, mjini Manila, wakati wa ziara rasmi ya siku mbili, wakati akieleza uhusiano wa mataifa yote mawili kuwa kwenye “enzi ya dhahabu.” Kishida ameeleza wasi wasi wa mataifa yote mawili kuhusiana na taharuki kwenye bahari ya East China Sea, na South China Sea, ambako Tokyo na Manila wamekuwa wakizozania na China.

Bila kutaja China moja kwa moja, taarifa hizo zimekuja kufuatia mizozo kadhaa kwenye bahari ya South China Sea, vikiwemo visa viwili vya ajali kati ya meli za China na Ufilipino mwezi uliopita. Malina ililaumu Beijing kwa kugonga boti zake kwa makusudi, wakati Japan ikikemea matukio hayo na kusema kwamba itasimama na Ufilipino katika kuhakikisha sheria za bahari zinaheshimiwa. Japan pia ina mipango sawa na hiyo na Uingereza na Australia, wakati Ufilipino pia ikishirikiana na Australia na Marekani.