Hezbollah yadai kushambulia kituo cha kijeshi cha Israel

Picha iliyorushwa na televisheni ya Hezbollah ya al-Manar TV January 5, 2024, ikionyesha kiongozi wa kundi hiloHassan Nasrallah akitoa hotuba kwa njia ya televisheni.

Kundi la wanamgambo la Hezbollah kutoka Lebanon limesema Jumamosi kwamba limerusha zaidi ya roketi 60 kwenye kituo kumoja cha kijeshi cha Israel.

Shambulizi hilo ni majibu kutokana na kuuawa kwa mmoja wa viongozi wake, Saleh al Arouri, mapema wiki hii, Hezbollah limesema kupitia taarifa. Kundi hilo linaamini kuwa Israel ilihusika kwenye kifo hicho, ingawa kufikia sasa haijakiri kuhusika.

Ijumaa kiongozi wa Hezbollah alisema kwamba ni lazima kundi lake lingejibu shambulizi hilo. “Hatuwezi kunyamaza kuhusu ukiukaji mkubwa hivi,” amesema Hassan Nasrallah, kulingana na shirika la habari la AP. Ameongeza kusema kwamba gharama ya kunyamaza ni kubwa kushinda hatari ya kujibu shambulizi hilo.

Kundi la Hamas pamoja na maafisa wa usalama wanadai shambulizi lililoua Saleh al- Arouri, kwamba lilitekelezwa na droni ya Israel, ingawa Israel haijasema lolote kutokana na madai hayo.

Hezbollah, sawa na Hamas, likiwa linaungwa mkono na Iran, na ambalo limeorodheshwa kuwa la kigaidi na Marekani pamoja na washirika wake, limekuwa likirusha roketi kwenye mpaka wa kaskazini wa Israel, tangu kuzuka kwa vita kati ya Israel na Hamas Oktoba mwaka uliopita.