Ghasia Kaskazini Mashariki mwa India zapelekea tofauti za kisiasa kati ya Waziri Mkuu na Upinzani

Waziri Mkuu wa India Narendra Modi .

Ghasia zilizozuka Mei kwenye jimbo la kaskazini mashariki mwa India la Maipur, zimesababisha mgawanyiko  kati ya jamii mbili  na kupelekea tofauti kubwa za kisiasa kati ya waziri mkuu Narendra Modi na vyama vya siasa.

Miezi mitatu baada ya magenge ya watu kushambulia miji na vijiji, hali ya taharuki imeendelea kutanda kati ya jamii ya Meiteis, ambao wengi ni wahindu, na wa Kuki, pamoja na makabila mengine ambao ni wa kristo. Tangu wakati huo maelfu ya maafisa wa usalama wamekuwa wakishika doria kwenye jimbo hilo lenye milima, karibu na mpaka wa Myanmar.

Kufikia sasa takriban watu 140 wamekufa kutokana na ghasia hizo, wakati mamia ya nyumba zilichomwa, huku takriban watu 60,000 wamekoseshwa makazi na kulazimika kuishi kwenye kambi za wakimbizi katika jimbo hilo lenye wakazi milioni 3.2.

Miongoni mwa watu waliotoroka makwao ni wazazi na wanafamilia wengine, wa Hoihnu Hauzel, anayeishi kwenye mji wa Gurugram, karibu na New Delhi, aliyeambia VOA kwamba jamaa zake walishambuliwa na magenge ya watu kwenye mji mkuu wa jimbo wa Imphal.