Biden na Zelensky wamezungumza kwa simu juu ya hali ya vita nchini Ukraine

Rais Joe Biden wa Marekani (L) na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy

Biden amethibitisha uungaji mkono usioyumba wa Marekani kwa Ukraine, ikiwa ni pamoja na kuendelea kwa usalama, uchumi na misaada ya kibinadamu, kulingana na taarifa iliyotolewa na White House siku ya Jumapili

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy amezungumza kwa njia ya simu na Rais wa Marekani Joe Biden kuhusu hali ya sasa ya vita nchini Ukraine.

Biden amethibitisha uungaji mkono usioyumba wa Marekani kwa Ukraine, ikiwa ni pamoja na kuendelea kwa usalama, uchumi na misaada ya kibinadamu, kulingana na taarifa iliyotolewa na White House siku ya Jumapili.

Viongozi hao pia walijadili matukio ya hivi karibuni nchini Russia, taarifa hiyo ilisema. Matukio ya Jumamosi yalifichua udhaifu wa utawala wa Putin, Zelenskyy alisema wakati wa mazungumzo yake ya simu na Biden.

Rais wa Ukraine amesema dunia lazima iweke shinikizo kwa Russia hadi pale utaratibu wa kimataifa utakaporejeshwa. Wawili hao walijadili njia za kutekeleza Mfumo wa Amani wa Ukraine, na nafasi zao kwenye mkutano ujao wa NATO huko Vilnius, Lithuania, hapo Julai 11 hadi 12.

Wakati huo huo, changamoto isiyo ya kawaida kwa Rais wa Russia, Vladimir Putin na wapiganaji kutoka vikosi vya jeshi la Wagner imefichua mapambano mapya katika nguvu ya uongozi wa Putin ambayo inaweza kuchukua wiki au miezi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken, alisema Jumapili katika mahojiano ya televisheni kwenye kipindi cha NBC cha Meet the Press.