Biashara kati ya China na Russia yaripotiwa kuongezeka tangu uvamizi wa Ukraine

Picha ya mkontena ya mizigo kwenye bandari moja ya Russia.

Biashara kati ya China na Russia mwaka 2023 imeripotiwa kuvunja rekodi kulingana na takwimu rasmi zilizotolewa leo na Beijing, huku biashara na Marekani ikishuka kwa mara ya kwanza ndani ya miaka 4, wakati mivutano ya kieneo na kisiasa ikiendelea kuongezeka.

Biashara kati ya China na Russia imeripotiwa kufikia zaidi ya dola bilioni 240, kulingana na takwimu za idara ya ushuru, kiwango ambacho kimepita dola bilioni 200 zilizokisiwa na mataifa hayo wakati wa kikao cha pamoja mwaka uliopita.

Kiwango hicho ndicho kikubwa zaidi kati ya mataifa hayo ambayo uhusiano wao unaonekana kushamiri kiuchumi na kisiasa tangu Moscow ilipofanya uvamizi wa Ukraine mwaka 2022. Beijing imekuwa ikikosolewa na mataifa ya magharibi kutokana na msimamo wake kuhusu uvamizi wa Ukraine, licha ya kusisitiza kwamba haiungi mkono upande wowote.

Hata hivyo imejiepusha kuikosoa Russia moja kwa moja. Kulingana na takwimu za Ijumaa, biashara kati ya mataifa hayo mawili imeongezeka kwa asilimia 26.3, wakati biashara kati ya Marekani na China ikiripotiwa kushuka kwa asilimia 11.6 kuanzia 2022.