Ajali ya mgodi wa dhahabu Tanzania yauwa watu 22

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametuma salama za rambi rambi  kwa ndugu jamaa na marafiki akisema vyombo vya ulinzi na usalama vinaendelea na juhudi za kutafuta miili.

Kuanguka kwa  mgodi mdogo wa dhahabu usio halali kumesababisha vifo vya takriban watu 22 kaskazini mwa Tanzania kufuatia mvua kubwa iliyonyesha, afisa mkuu mmoja wa serikali alisema Jumapili.

Kuanguka kwa mgodi mdogo wa dhahabu usio halali kumesababisha vifo vya takriban watu 22 kaskazini mwa Tanzania kufuatia mvua kubwa iliyonyesha, afisa mkuu mmoja wa serikali alisema Jumapili.

Ajali hiyo ilitokea mapema Jumamosi katika mkoa wa Simiyu baada ya kundi la watu wenye umri wa kati ya miaka 24 na 38 kuanza uchimbaji wa madini katika eneo ambalo shughuli zilikuwa zimezuiliwa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha, Mkuu wa Wilaya ya Bariadi mkoani humo, Simon Simalenga, aliliambia shirika la habari la Reuters.

Awali tuliambiwa kuna watu 19 hadi 20 ambao wamekwama kwenye mgodi lakini kwa bahati mbaya tuliishia kuopoa miili 22 alisema na kuongeza kuwa zoezi la utafutaji na uokoaji linaendelea japo karibu vifusi vyote vilivyokuwa vimewafukia sasa vimeondolewa.

Simalenga alisema kikundi hicho kiligundua eneo lenye madini mengi takribani wiki mbili hadi tatu zilizopita na kuhamia na kuanza uchimbaji kabla ya serikali kuidhinisha usalama na taratibu za kimazingira.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametuma salama za rambi rambi kwa ndugu jamaa na marafiki akiandika kwenye mtandao wa X “nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya vifo vya watu zaidi ya 21 kufuatia ajali ya kufunikwa na ardhi katika Mgodi wa Ng'alita, Wilaya ya Bariadi, mkoani Simiyu. Ndugu zetu hawa walikuwa wachimbaji wadogo katika eneo hili, wakijitafutia riziki zao, familia zao na kuchangia maendeleo ya taifa letu”.

Akiongeza kwamba vyombo vya ulinzi na usalama vikishirikiana na uongozi wa mkoa vinaendelea na juhudi za kutafuta miili mingine ambayo bado imekwama ndani ya vifusi.