Tanzania bado inafuata misingi ya Ujamaa:Butiku.

Mwalimu Julius K.Nyerere muasisi wa taifa la Tanzania.

Watanzania wamekumbushana kufuata misingi ya amani, umoja na maendeleo yaliyokuwa yakihubiriwa na baba wa taifa la Tanzania Mwalimu Julius Nyerere wanapoadhimisha miaka 14 tangu kufariki kwa kiongozi huyo Oktoba 14, 1999.

Mkurugenzi wa taasisi ya Mwalimu Nyerere, Bw. Joseph Butiku akizungumza na Sauti ya Amerika amesema nchi hiyo inamkumbuka Mwalimu Nyerere kama mzalendo aliyetetea maslahi ya nchi hiyo na bara zima la Afrika, alikuwa mpigania uhuru wa taifa hilo na Afrika kwa jumla pamoja na kuwa mtetezi wa wanyonge, mpigania usawa.

Bw.Batiku anasema Mwalimu Nyerere aliweka misingi muhimu ya maendeleo katika fani za elimu, kilimo, umoja wa taifa na muungano.
Akijibu ikiwa misingi na nadharia ya mwalimu Nyerere inafuatwa, anasema pamoja na changamoto za hapa na pale bado anaamini inafuatwa, na kwamba sera ya Ujamaa na kujitegemea inafuatwa kwani kwa wanaofahamu Ujamaa ni kujali utu na heshima na haki ya kila mtu na kwamba kila mtu aweze kupata elimu, afya, nafasi ya kuishi na usawa.

Bw. Butiku, amesema kwamba nchi hiyo ina enzi na kufuata mpaka sasa misingi hiyo ya kijamaa ila utaratibu wa kutekeleza ndio jambo la tofauti akisema kwamba hapo ndio wanaweza kutofautiana hapa na pale lakini mwelekeo wa serikali ya nchi hiyo na watu wake ni ule ule.

Mwalimu Nyerere alifariki Oktoba 14 ,1999 huko London Uingereza kutokana na ugonjwa wa kansa ya damu.