Washambuliaji wasiojulikana waliokuwa na silaha wamewaua wanajeshi 11 wa Burkina Faso na kuwajeruhi wengine wanane katika mkoa wa Est nchini Burkina Faso siku ya Jumapili vyanzo vine vya jeshi la serikali vililiambia shirika la habari la Reuters.
Mkoa huo ni miongoni mwa maeneo yaliyokumbwa na ongezeko la ukosefu wa usalama huku makundi ya wanajihadi yenye uhusiano na al-Qaeda na Islamic State yakijaribu kupata udhibiti wa maeneo ambayo yaliwahi kuwa na amani katika eneo la Central Sahel huko Afrika magharibi.
Vyanzo hivyo havikutoa taarifa zaidi juu ya shambulizi la karibuni na hakukuwa na maoni ya haraka kutoka serikalini. Utawala wa kijeshi ulikamata mamlaka katika mapinduzi ya Januari dhidi ya Rais Roch Kabore wakimlaumu kwa kushindwa kudhibiti ghasia zinazoongezeka za wanamgambo wa kiislam ambao wameua maelfu ya watu na kuwalazimisha zaidi ya watu milioni mbili kukimbia nyumba zao katika Sahel.