Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Septemba 17, 2024 Local time: 06:14

Watu 129 wauawa katika jaribio la kutoroka gerezani huko DRC


Familia za wafungwa zikiwa nje ya gereza la Makala, Kinshasa kutaka taarifa kuhusu hali za ndugu zao Septemba 3, 2024. Picha na AFP
Familia za wafungwa zikiwa nje ya gereza la Makala, Kinshasa kutaka taarifa kuhusu hali za ndugu zao Septemba 3, 2024. Picha na AFP

Jaribio la kutoroka katika gereza kuu la Congo limesababisha vifo vya watu 129, wakiwemo baadhi waliopigwa risasi na wengine walikufa katika mkanyagano kwenye gereza hilo lenye msongamano mkubwa, mamlaka ilisema Jumanne.

Wanaharakati walisema idadi ya vifo ni kubwa zaidi lakini hawakutoa takwimu kamili.

Tathmini ya awali ilionyesha kuwa wafungwa 24 waliuawa kwa "risasi za maonyo" zilizofyatuliwa na walinzi wakati wafungwa walipojaribu kutoroka kutoka Gereza Kuu la Makala katika mji mkuu wa Kinshasa mapema Jumatatu, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Congo, Jacquemin Shabani, alisema kwenye mtandao wa kijamii wa X.

"Kuna pia watu 59 waliojeruhiwa ambao wanahudumiwa na serikali, pamoja na baadhi ya matukio ya wanawake kubakwa," alisema, akiongeza kuwa utulivu sasa umerejeshwa gerezani, sehemu ya gereza hilo ilikuwa imeteketea kwa moto wakati wa jaribio hilo la kutoroka.

Hakutoa maelezo zaidi juu ya matukio ya ubakaji. Gereza hilo lina wafungwa wanaume na wanawake.

Haikujulikana kama watu wote 129 waliopoteza maisha walikuwa wafungwa. Pia, haijajulikana mara moja jinsi mkanyagano ulivyotokea kwani maelezo ya jaribio la kutoroka ni machache.

Makala, gereza kubwa zaidi nchini DRC lenye uwezo wa kuhifadhi watu 1,500, lina zaidi ya wafungwa 12,000, wengi wao wakiwa wanasubiri kesi zao, kulingana na ripoti ya hivi karibuni ya Amnesty International kuhusu nchi hiyo.

Gereza hilo limewahi kushuhudia majaribio ya kutoroka, ikiwa ni pamoja na mwaka 2017 ambapo wanachama wa dhehebu la kidini walivamia gereza na kuwaachilia huru wafungwa kadhaa.

Milio ya risasi ndani ya gereza ilianza takriban saa sita usiku Jumapili na ikadumu hadi Jumatatu asubuhi, wakazi wa eneo hilo walisema.

Forum

XS
SM
MD
LG