Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 18, 2024 Local time: 10:29

Wanajeshi wa MONUSCO wawekwa kizuizini DRC kwa tuhuma za unyanyasaji kijinsia


Baadhi ya wanajeshi wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa waliopo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (MONUSCO) ukiwa Goma Agosti 1, 2022. Picha na ALEXIS HUGUET / AFP.
Baadhi ya wanajeshi wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa waliopo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (MONUSCO) ukiwa Goma Agosti 1, 2022. Picha na ALEXIS HUGUET / AFP.

Wanajeshi wanane wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa waliokuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamewekwa kizuizini kwa madai ya unyanyasaji wa kijinsia.

Vyanzo vililiambia shirika la habari la Reuters siku ya Alhamisi, wakati Umoja wa Mataifa ukisema kuwa utachunguza utovu mkubwa wa nidhamu bila kuutaja.

Ujumbe wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa Mashariki mwa Congo, unaojulikana kama MONUSCO, ulisema katika taarifa yake kuwa umewasimamisha kazi wanajeshi wake kadhaa wa kulinda amani kutokana na taarifa za utovu wa nidhamu, ujumbe huo haukutoa maelezo zaidi.

Chanzo cha Umoja wa Mataifa na chanzo cha usalama cha Congo vilisema madai hayo yanawahusu walinda amani wanane wa Afrika Kusini waliokuwa katika mji wa Mashariki wa Beni. Vyanzo hivyo viwili vilizungumza kwa sharti la kutotajwa majina kwa sababu hawakuruhusiwa kulijadili suala hili na vyombo vya habari.

"Tumefahamishwa na wenzetu wa Umoja wa Mataifa kuwa wanajeshi wanane wa kulinda amani wa Afrika Kusini wamewekwa kizuizini kwa tuhuma za unyanyasaji wa kijinsia," kilisema chanzo cha usalama kilichopo Beni.

Chanzo cha Umoja wa Mataifa kilisema madai hayo yalihusisha madanguro yaliyoko jirani na kambi za kikosi cha Afrika Kusini.

Wasemaji kutoka idara ya ulinzi ya Afrika Kusini na wizara ya mambo ya nje na serikali ya Congo hawakuweza kujibu kwa haraka maombi ya maoni kuhusiana na suala hilo.

Katika miaka ya hivi karibuni, Umoja wa Mataifa umeunda vitengo maalum kupambana na unyanyasaji wa kijinsia na kusaidia waathirika, wakiwemo walioko Congo, lakini umekuwa na changamoto katika kukomesha tatizo hilo.

Chini ya mfumo wa sasa, Umoja wa Mataifa unaweza kuchunguza uhalifu na kuwarudisha walinda amani katika nchi zao, lakini hauna uwezo wa kushtaki.

Chanzo cha habari ni Shirika la habari la Reuters

Forum

XS
SM
MD
LG