Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Mei 10, 2024 Local time: 19:21

Joto kali lasababisha shule kufungwa Sudan


mji wa Juba wakati jua linapozama. Picha na REUTERS/Adriane Ohanesian
mji wa Juba wakati jua linapozama. Picha na REUTERS/Adriane Ohanesian

Sudan Kusini, taifa changa zaidi duniani, inakumbwa na wimbi la joto kali, na kusababisha serikali kuamuru kufungwa kwa shule zote kwa wiki mbili.

Wakaazi wa mji mkuu wa Juba wanakabiliwa na ongezeko kubwa la bei ya barafu na maji huku mahitaji yakiongezeka kutokana na joto hilo.

Uwamuzi wa kufunga shule umeungwa mkono zaidi na walimu, akiwemo Anthony Moi-Alamin, mkuu wa shule ya Juba, ambaye alikiri ni vigumu kudumisha mazingira mazuri ya kujifunzia wakati wa joto kali kama hilo.

"Ni kali sana, linaathiri sana mazingira ya kusoma, kwani wakati kama huu huwezi kukaa darasani, watoto wanatokwa na majasho darasani, walimu nao wanatokwa na majasho, kuna watoto wengi darasani, hivyo hali ya msongamano sio nzuri wakati wa joto."alisema Moi-Alamin.

Kwa upande mwengine Emmanuel Bidal Martin, dereva wa Bajaji na mzazi, anaeleza kwamba anahisia mchanganyiko kutokana na uamuzi wa serikali.

“Ni uamuzi mzuri wa serikali kuwarudisha watoto nyumbani kwa sababu kuwaweka sehemu moja kwenye joto hili kunaweza kusababisha magonjwa, lakini kuwaweka nyumbani pia ni hatari, haswa wakati hakuna watu wazima wa kuwaangalia. Watacheza kwenye jua” alisema Bidal Martin.

Ingawa amefarijika kwamba watoto wake wanalindwa dhidi ya kuathiriwa na hali mbaya ya hewa kwa kufungwa kwa shule huku hali ya joto ikitarajiwa kupanda hadi nyuzi joto 45 Celsius, lakini bado ana wasiwasi kwani hakutakuwa na mtu wa kuwatunza watoto nyumbani.

Joto hilo pia linaathiri wagonjwa hospitalini kulingana na maafisa wa uuguzi na wanasema joto linaweza kusababisha hatari kwa afya ya wagonjwa na raia wa kawaida hasa wale ambao hawatapata maji ya kunywa ya kutosha.

Forum

XS
SM
MD
LG