Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatatu, Mei 20, 2024 Local time: 22:19

Idara ya Usalama Somalia yadai taifa la kigeni limehusika na mlipuko wa bomu


Waokoaji kutoka Uturuki wakishirikiana na wale wa Somalia kuwapeleka ndani ya ndege kwa ajili ya kusafirishwa kwenda kupata matibabu Uturuki Disemba 2019. (Foto: AFP)
Waokoaji kutoka Uturuki wakishirikiana na wale wa Somalia kuwapeleka ndani ya ndege kwa ajili ya kusafirishwa kwenda kupata matibabu Uturuki Disemba 2019. (Foto: AFP)

Idara ya Usalama wa Taifa ya Somalia imeishutumu nchi ya kigeni bila ya kuitaja jina kwa kupanga shambulizi la bomu lililokuwa katika lori ambalo liliuwa watu wasiopungua 80 mjini Mogadishu Jumapili usiku.

“Tumewasilisha ripoti ya awali kwa viongozi wa kitaifa inayoonyesha kuwa shambulizi hilo dhidi ya watu wa Somalia mjini Mogadishu Disemba 28, 2019 ulipangwa na taifa la kigeni,” Idara ya Usalama wa Taifa na Ulinzi ya Somalia (NSA) imeeleza katika ujumbe wa tweet iliyotuma Jumatatu.

“Ili kukamilisha uchunguzi unaoendelea tutaomba ushirikiano kutoka kwa baadhi ya idara mbalimbali za usalama wa taifa duniani.”

Idara ya Usalama wa Taifa

NISA haikutaja nchi inayoituhumu kuhusika na shambulio la bomu, na wala haikutoa ushahidi kuthibitisha madai yake.

Madai hayo yanaelekea kukinzana na tamko la awali lililotolewa na viongozi wa serikali kuu ya Somalia.

Rais wa Somalia

Rais Mohamed Abdullahi Farmajo Jumamosi aliwalaumu al-Shabab, akisema kikundi hicho cha wapiganaji kilikuwa na lengo la kuuwa raia na watoto

“Al-Shabab hawatengenzi kitu, kazi yao nikuharibu,” amesema. “Hawajengi shule, vituo vya afya, wala kuwalisha watoto – wameingia mkataba wa kuzuia maendeleo na kuuwa watu na watoto wa taifa la Somalia.

Al-Shabab hawakudai kuhusika na shambulio hilo lakini wachambuzi na viongozi wengine wa Somalia wamelaumu wale waliokuwa na misimamo mikali kufanya shambulizi. Kikundi hicho hakikudai kuhusika na mashambulio ya nyuma likiwemo lile la Octoba 14, 2017 ambapo watu 587 waliuawa mjini Mogadishu.

Mahakama

Mahakama mmoja nchini Somalia imemkuta na hatia mwanachama wa kikundi cha al-Shabab kwa kuratibu shambulio hilo.

Mtu huyo, ambaye aliwahi kipindi Fulani kuwa dereva wa kiongozi wa hivi sasa wa al-Shabab alikutikana na makosa na kuhukumiwa kifo mwaka 2018.

Wanasiasa wa upinzani wameituhumu NISA “kwa kuupotosha umma” katika tuhuma za hivi karibuni.

Abdirahman Abdishakur wa Chama cha Wadajir ameandika : “Kwa NISA kudai kuwa nchi ya kigeni ilikuwa nyuma ya shambulizi hilo… siyo tu inapotosha umma na inakwepa udhaifu wake, lakini pia inahamisha lawama kutoka kwa gaidi. Huu ni ushirikiano wa wazi na al-Shabab.

Mchambuzi

Mchambuzi Abdirashid Khalif Hashi amesema serikali isitume madai kama haya kupitia ujumbe wa tweet bila ya kutoa maelezo Zaidi.

“NISA ni lazima itoe maelezo Zaidi,”amesema. “Hii ni habari kubwa, viongozi wa kitaifa akiwemo rais, waziri mkuu, waziri wa usalama wa taifa, bunge ni lazima waitisha mkutano wa waandishi wa habari na kuzungumza iwapo nchinyingine zilikuwa nyuma ya tukio hili.

Sauti ya Amerika haikuweza kumpata Waziri wa Usalama kutoa maelezo juu ya hilo, ambaye anasimamia idara hiyo.

XS
SM
MD
LG